0


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime
Ripoti ya uchunguzi wa kashfa ya kampuni ya kufua umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) ya uchotwaji wa Sh. bilioni 306 kwenye akaunti ya Tegeta Escrow, iliyoko Benki Kuu ya Tanzania (BoT) zimeibwa na kuzua mambo.

Kufuatia tukio hilo, Jeshi la Polisi mkoani Dodoma limewatia mbaroni vijana wawili wanaotuhumiwa kusambaza mitaani ripoti ‘feki’ ya ukaguzi wa hesabu za fedha hizo uliofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhusiana na kashfa hiyo.

Ripoti hiyo inadaiwa kuibwa na vijana hao katika Ofisi ya Katibu wa Bunge na kuichakachua kabla ya kuisambaza mitaani.

Vijana hao, ambao wanadaiwa kuwa ni baadhi ya watu waliomo katika kikosi cha waziri mmoja kilichoingia mjini Dodoma, wanadaiwa kusambaza ripoti hiyo ‘feki’ kwa kutumwa na waziri huyo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime, alithibitisha polisi kuwashikilia vijana hao tangu juzi na kusema kuwa walipohojiwa, walikiri kupewa nyaraka hizo na mbunge, ambaye hata hivyo alikataa kumtaja kwa sababu za kiuchunguzi.

Pia Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashililah, alithibitisha kutoa taarifa polisi kuhusu vijana hao kumiliki nyaraka zenye mhuri ya ofisi yake isivyo halali.

Kamanda Misime alisema hadi jana walikuwa wanawashikilia vijana hao. “Jana (juzi), tulipata taarifa kutoka kwa Katibu wa Bunge kuwa kuna watu wanasambaza nyaraka kutoka Ofisi ya Katibu wa Bunge,” alisema Misime na kuongeza: “Baada ya taarifa hiyo, tulianza msako katika mji huu wa Dodoma na kufanikiwa kuwakamata vijana wawili.”
“Mmoja  tulimkuta akiwa na nyaraka tatu, ambazo mbili zilikuwa na muhuri wa Ofisi ya Katibu wa Bunge.”

“Tulikwenda hadi katika hoteli aliyofikia na kufanya uchunguzi na tulipombana zaidi, alikiri kupewa na mbunge mmoja, ambaye kwa sasa jina lake tunalihifadhi kwa sababu ya uchunguzi.”

“Hatua tunayochukua sasa ni kuzipeleka karatasi hizi kwa mtaalamu wa maandishi kwa uchunguzi zaidi. Swali la kujiuliza kama zilikuwa za siri, je, huyu kijana alizipataje na kuanza kuzagaa mitaani?” alihoji Kamanda Misime.

Wakati vijana hao wakishikiliwa na polisi, hali bado ni tete ndani ya Bunge la Jamhuri wa Muungano wa Tanzania. Hiyo ni utokana na kuibuka madai kadhaa, ikiwamo kusukwa kwa mipango inayoelezwa kuwa ni ya hujuma ili kukwamisha uwasilishaji wa ripoti sahihi ya uchunguzi wa kashfa hiyo.

Tangu lilipoanza Bunge hadi ilipokabidhi ripoti hiyo, kumeibuka mapambano na hata kugawanyika kwa wabunge, huku kundi moja likitaka iwasilishwe bungeni na lingine likipinga.

Chanzo cha kuaminika kiliiambia NIPASHE jana kuwa baada ya kuibuliwa madai ya kuibwa nyaraka za ripoti hiyo katika Ofisi ya Katibu wa Bunge pamoja na kunyofolewa baadhi ya kurasa, makundi hayo yamekuwa yakipanga mikakati ya kila aina.

Imeelezwa kuwa mmoja wa waziri anadaiwa amekuwa akipinga kuwasilishwa kwa ripoti hiyo bungeni akidaiwa kuwatumia baadhi ya wabunge.
“Tangu ilipowasilishwa ripoti ya CAG pamoja na ile ya Takukuru hapa Dodoma, hali siyo shwari. Maana kati yetu wabunge, hasa wa CCM tumekuwa hatuaminiani tena… na sasa waziri (jina tunalo) ndiyo amekuwa akitajwa kusuka mikakati ya kuiba ripoti ya uchunguzi katika Ofisi ya Katibu wa Bunge,” kilisema chanzo hicho. 

Kiliongeza: “Lakini hili halisaidii. Ni lazima ripoti isomwe na wezi waliokula fedha hizi za walipakodi wachukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria. Na kama ilivyo kwa wezi wengine.

Juzi Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni iliibuka na kutoa taarifa za kuzagaa kwa nyaraka hiyo ya CAG, ambayo bado inafanyiwa kazi ya kiuchunguzi na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC).

Mwenyekiti Mwenza wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), James Mbatia, alisema ripoti iliyonaswa ikizagaa mitaani ni ile, ambayo CAG kupitia Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, aliikabidhi kwa Katibu wa Bunge. Mbali na hilo, alisema ripoti hiyo imenyofolewa baadhi ya kurasa kwa lengo la kupotosha ukweli kwa umma kutokana na uzito wa suala hilo.

“Kurasa ya 57, 58 na 59 zimenyofolewa na kundi la maharamia, ambao wamepiga kambi hapa Dodoma kwa ufadhili wa kigogo mmoja kutoka wzara ya nishati na madini,” alisema Mbatia.

Aliongeza: “Mkakati wao ili ionekane kuwa haifai kuingizwa bungeni kutokana na kile wanachotaka kudai kuwa imeshatoka mbele ya umma na siyo siri tena kwa hili, hatukubali hata kidogo, na tunataka Jumatatu iingie bungeni.”

“Asubuhi Jumatatu (leo), tutakutana wabunge wote wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na kutoka na azimio, ambalo tutaliwasilisha bungeni kuhusu suala hili,” alisema Mbatia.

CAG AZUNGUMZA
Wakati kukiwapo na taarifa za kuchakachuliwa kwa ripoti ya Escrow, Ofisi ya CAG) imesema kuwa ripoti yake ya ukaguzi iliyowasilisha kwa ofisi ya Bunge haikuchakachuliwa.

Kaimu CAG, Francis Mwakapalila, alisema hayo jana wakati akizungumza na NIPASHE iliyotaka kujua kuwepo kwa taarifa kuwa kuna kurasa tatu ambazo zimeondolewa katika ripoti ya CAG kuhusu kashfa ya IPTL.

Tamko hilo la CAG limekuja siku moja tu baada ya Mbatia, kueleza kuwa ukurasa wa 57,58 na 59 ambazo zimebeba mambo ya msingi zimenyofolewa katika ripoti hiyo.  “Mimi sijaiona hiyo ripoti inayodaiwa kunyofolewa kurasa, ningeiona ningelinganisha na ile niliyopeleka katika ofisi za Bunge kama ni yenyewe, lakini niliyowasilisha kwa wahusika ilikuwa na ‘page’ zote,” alisema.

 Wakati Kaimu CAG akieleza hivyo, zipo taarifa kuwa wakati wa kikao cha Kamati ya Uongozi wa Bunge, ofisi ya CAG ilipoulizwa kuhusu kutokuwapo kwa kurasa ilieleza kuwa ni kwasababu kurasa hizo ziliondolewa na kuingizwa katika ripoti ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).  Chanzo cha habari kutoka katika kikao hicho kieleza kuwa kurasa hizo zilizoondolewa zilikuwa na majina ya watu wanaotuhumiwa kuhusika na uchotwaji wa fedha hizo na hivyo kupelekwa Takukuru ili kuruhusu hatua zaidi za kisheria zichukuliewe dhidi ya wahusika.

PINDA: SERIKALI IJIPANGE
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alisema serikali inapaswa kujipanga vizuri juu ya kinachoendelea ili itoe majibu yanayoridhisha kwa umma kuhusiana na suala hilo la IPTL.
Alisema hayo jana katika sherehe za kuwekwa wakfu Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Kati,  Dk. Dickson Chilongani, mjini Dodoma jana.

Alisema Watanzania wanapita kipindi kibaya kuelekea uchaguzi mkuu, kwani kuna kampeni chafu za kila aina za kuchafuana.

“Baba Askofu kipindi hiki ni kibaya, tunasema lala salama. Watu wengi wamekuwa wakichafuana kwa ajili ya kutaka kupata madaraka. Kubwa ni serikali kutoa maelezo yatakayotuaminisha kwa wananchi. Ila uadilifu mkubwa unahitajika serikalini kwa sababu kuna mapesa,” alisema Pinda.

PROF. MWANDOSYA
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya, alisema chama (CCM) wanaendelea na vikao kujadili juu ya kashfa hiyo na kwamba, ni lazima ripoti ya uchunguzi iwekwe hadharani ili mbivu na mbichi zijulikane. 

Alisema hayo akijibu swali aliloulizwa na mmoja wa wanafunzi wanachama wa CCM wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) aliyetaka kujua nini maoni yake juu ya watu wanaokichafua chama kupitia kashfa ya IPTL.

Mimi binafsi ninachoweza kusema watu wote wanaotajwa kuhusiia na suala la IPTL ni vema wakakaa pembeni ili kuepuka kukipaka chama matope,” alisema Profesa Mwandosya.

NAPE: HATUTAMBEBA MTU
Katika hatua nyingine, wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye, amesema kila mtu atabeba mzigo wake katika kashfa ya Escrow.

Alisema huo ni msimamo wa chama kuwa, kila aliyehusika katika sakata hilo abebe msalaba wake  na akiache chama salama.

Nape alitoa kauli hiyo jana, wakati akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Ilulu wilaya ya Lindi, katika kuhitimisha ziara ya siku nane ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, katika mkoa wa Lindi.

“Chama chetu kiko imara na kinafuata kanuni na taratibu zake za kuwawajibisha wale wanaokosea ndani ya chama, skendo zote za rushwa mnazoziskia huko tunashughulika nazo, hata hili sakata linaloendelea huko bungeni la Escrow, msimamo wa chama ni kuwawaliohusika waondoke waache chama kikiwa salama,” alisema Nape.

Alisema chama hicho kinafuata maadili kanuni na miiko ya uongozi iliyopo kwenye katiba hivyo hakiwezi kulea uovu.

Nape alitolea mfano wa utendaji kazi ndani ya chama hicho katika sakata la Richmond, ambalo lilisababisha aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa na mawaziri wengine wawili kujiuzulu.

Habari : Muhibu Said, Dodoma;  Thobias Mwanakatwe, Dar 
na Mary Godfrey, Lindi.
CHANZO: NIPASHE

Post a Comment

 
Top