Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime
Ripoti ya
uchunguzi wa kashfa ya kampuni ya kufua umeme ya Independent Power
Tanzania Limited (IPTL) ya uchotwaji wa Sh. bilioni 306 kwenye akaunti
ya Tegeta Escrow, iliyoko Benki Kuu ya Tanzania (BoT) zimeibwa na kuzua
mambo.
Kufuatia
tukio hilo, Jeshi la Polisi mkoani Dodoma limewatia mbaroni vijana
wawili wanaotuhumiwa kusambaza mitaani ripoti ‘feki’ ya ukaguzi wa
hesabu za fedha hizo uliofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za
Serikali (CAG) kuhusiana na kashfa hiyo.
Ripoti hiyo inadaiwa kuibwa na vijana hao katika Ofisi ya Katibu wa Bunge na kuichakachua kabla ya kuisambaza mitaani.
Vijana hao,
ambao wanadaiwa kuwa ni baadhi ya watu waliomo katika kikosi cha waziri
mmoja kilichoingia mjini Dodoma, wanadaiwa kusambaza ripoti hiyo ‘feki’
kwa kutumwa na waziri huyo.
Kamanda wa
Polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime, alithibitisha polisi kuwashikilia
vijana hao tangu juzi na kusema kuwa walipohojiwa, walikiri kupewa
nyaraka hizo na mbunge, ambaye hata hivyo alikataa kumtaja kwa sababu za
kiuchunguzi.
Pia Katibu
wa Bunge, Dk. Thomas Kashililah, alithibitisha kutoa taarifa polisi
kuhusu vijana hao kumiliki nyaraka zenye mhuri ya ofisi yake isivyo
halali.
Kamanda
Misime alisema hadi jana walikuwa wanawashikilia vijana hao. “Jana
(juzi), tulipata taarifa kutoka kwa Katibu wa Bunge kuwa kuna watu
wanasambaza nyaraka kutoka Ofisi ya Katibu wa Bunge,” alisema Misime na
kuongeza: “Baada ya taarifa hiyo, tulianza msako katika mji huu wa
Dodoma na kufanikiwa kuwakamata vijana wawili.”
“Mmoja tulimkuta akiwa na nyaraka tatu, ambazo mbili zilikuwa na muhuri wa Ofisi ya Katibu wa Bunge.”
“Tulikwenda
hadi katika hoteli aliyofikia na kufanya uchunguzi na tulipombana zaidi,
alikiri kupewa na mbunge mmoja, ambaye kwa sasa jina lake tunalihifadhi
kwa sababu ya uchunguzi.”
“Hatua
tunayochukua sasa ni kuzipeleka karatasi hizi kwa mtaalamu wa maandishi
kwa uchunguzi zaidi. Swali la kujiuliza kama zilikuwa za siri, je, huyu
kijana alizipataje na kuanza kuzagaa mitaani?” alihoji Kamanda Misime.
Wakati
vijana hao wakishikiliwa na polisi, hali bado ni tete ndani ya Bunge la
Jamhuri wa Muungano wa Tanzania. Hiyo ni utokana na kuibuka madai
kadhaa, ikiwamo kusukwa kwa mipango inayoelezwa kuwa ni ya hujuma ili
kukwamisha uwasilishaji wa ripoti sahihi ya uchunguzi wa kashfa hiyo.
Tangu
lilipoanza Bunge hadi ilipokabidhi ripoti hiyo, kumeibuka mapambano na
hata kugawanyika kwa wabunge, huku kundi moja likitaka iwasilishwe
bungeni na lingine likipinga.
Chanzo cha
kuaminika kiliiambia NIPASHE jana kuwa baada ya kuibuliwa madai ya
kuibwa nyaraka za ripoti hiyo katika Ofisi ya Katibu wa Bunge pamoja na
kunyofolewa baadhi ya kurasa, makundi hayo yamekuwa yakipanga mikakati
ya kila aina.
Imeelezwa
kuwa mmoja wa waziri anadaiwa amekuwa akipinga kuwasilishwa kwa ripoti
hiyo bungeni akidaiwa kuwatumia baadhi ya wabunge.
“Tangu
ilipowasilishwa ripoti ya CAG pamoja na ile ya Takukuru hapa Dodoma,
hali siyo shwari. Maana kati yetu wabunge, hasa wa CCM tumekuwa
hatuaminiani tena… na sasa waziri (jina tunalo) ndiyo amekuwa akitajwa
kusuka mikakati ya kuiba ripoti ya uchunguzi katika Ofisi ya Katibu wa
Bunge,” kilisema chanzo hicho.
Kiliongeza:
“Lakini hili halisaidii. Ni lazima ripoti isomwe na wezi waliokula fedha
hizi za walipakodi wachukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria. Na kama
ilivyo kwa wezi wengine.
Juzi Kambi
Rasmi ya Upinzani Bungeni iliibuka na kutoa taarifa za kuzagaa kwa
nyaraka hiyo ya CAG, ambayo bado inafanyiwa kazi ya kiuchunguzi na
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC).
Mwenyekiti
Mwenza wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), James Mbatia, alisema
ripoti iliyonaswa ikizagaa mitaani ni ile, ambayo CAG kupitia Waziri
Mkuu, Mizengo Pinda, aliikabidhi kwa Katibu wa Bunge. Mbali na hilo,
alisema ripoti hiyo imenyofolewa baadhi ya kurasa kwa lengo la kupotosha
ukweli kwa umma kutokana na uzito wa suala hilo.
“Kurasa ya
57, 58 na 59 zimenyofolewa na kundi la maharamia, ambao wamepiga kambi
hapa Dodoma kwa ufadhili wa kigogo mmoja kutoka wzara ya nishati na
madini,” alisema Mbatia.
Aliongeza:
“Mkakati wao ili ionekane kuwa haifai kuingizwa bungeni kutokana na kile
wanachotaka kudai kuwa imeshatoka mbele ya umma na siyo siri tena kwa
hili, hatukubali hata kidogo, na tunataka Jumatatu iingie bungeni.”
“Asubuhi
Jumatatu (leo), tutakutana wabunge wote wa Kambi Rasmi ya Upinzani
Bungeni na kutoka na azimio, ambalo tutaliwasilisha bungeni kuhusu suala
hili,” alisema Mbatia.
CAG AZUNGUMZA
Wakati
kukiwapo na taarifa za kuchakachuliwa kwa ripoti ya Escrow, Ofisi ya
CAG) imesema kuwa ripoti yake ya ukaguzi iliyowasilisha kwa ofisi ya
Bunge haikuchakachuliwa.
Kaimu CAG,
Francis Mwakapalila, alisema hayo jana wakati akizungumza na NIPASHE
iliyotaka kujua kuwepo kwa taarifa kuwa kuna kurasa tatu ambazo
zimeondolewa katika ripoti ya CAG kuhusu kashfa ya IPTL.
Tamko hilo
la CAG limekuja siku moja tu baada ya Mbatia, kueleza kuwa ukurasa wa
57,58 na 59 ambazo zimebeba mambo ya msingi zimenyofolewa katika ripoti
hiyo. “Mimi sijaiona hiyo ripoti inayodaiwa kunyofolewa kurasa,
ningeiona ningelinganisha na ile niliyopeleka katika ofisi za Bunge kama
ni yenyewe, lakini niliyowasilisha kwa wahusika ilikuwa na ‘page’
zote,” alisema.
Wakati
Kaimu CAG akieleza hivyo, zipo taarifa kuwa wakati wa kikao cha Kamati
ya Uongozi wa Bunge, ofisi ya CAG ilipoulizwa kuhusu kutokuwapo kwa
kurasa ilieleza kuwa ni kwasababu kurasa hizo ziliondolewa na kuingizwa
katika ripoti ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
Chanzo cha habari kutoka katika kikao hicho kieleza kuwa kurasa hizo
zilizoondolewa zilikuwa na majina ya watu wanaotuhumiwa kuhusika na
uchotwaji wa fedha hizo na hivyo kupelekwa Takukuru ili kuruhusu hatua
zaidi za kisheria zichukuliewe dhidi ya wahusika.
PINDA: SERIKALI IJIPANGE
Waziri Mkuu,
Mizengo Pinda, alisema serikali inapaswa kujipanga vizuri juu ya
kinachoendelea ili itoe majibu yanayoridhisha kwa umma kuhusiana na
suala hilo la IPTL.
Alisema hayo
jana katika sherehe za kuwekwa wakfu Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana
Dayosisi ya Kati, Dk. Dickson Chilongani, mjini Dodoma jana.
Alisema Watanzania wanapita kipindi kibaya kuelekea uchaguzi mkuu, kwani kuna kampeni chafu za kila aina za kuchafuana.
“Baba Askofu
kipindi hiki ni kibaya, tunasema lala salama. Watu wengi wamekuwa
wakichafuana kwa ajili ya kutaka kupata madaraka. Kubwa ni serikali
kutoa maelezo yatakayotuaminisha kwa wananchi. Ila uadilifu mkubwa
unahitajika serikalini kwa sababu kuna mapesa,” alisema Pinda.
PROF. MWANDOSYA
Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya, alisema
chama (CCM) wanaendelea na vikao kujadili juu ya kashfa hiyo na kwamba,
ni lazima ripoti ya uchunguzi iwekwe hadharani ili mbivu na mbichi
zijulikane.
Alisema hayo
akijibu swali aliloulizwa na mmoja wa wanafunzi wanachama wa CCM wa
Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) aliyetaka kujua nini maoni yake juu ya watu
wanaokichafua chama kupitia kashfa ya IPTL.
Mimi binafsi
ninachoweza kusema watu wote wanaotajwa kuhusiia na suala la IPTL ni
vema wakakaa pembeni ili kuepuka kukipaka chama matope,” alisema Profesa
Mwandosya.
NAPE: HATUTAMBEBA MTU
Katika hatua
nyingine, wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape
Nnauye, amesema kila mtu atabeba mzigo wake katika kashfa ya Escrow.
Alisema huo ni msimamo wa chama kuwa, kila aliyehusika katika sakata hilo abebe msalaba wake na akiache chama salama.
Nape alitoa
kauli hiyo jana, wakati akizungumza na wananchi katika mkutano wa
hadhara uliofanyika katika viwanja vya Ilulu wilaya ya Lindi, katika
kuhitimisha ziara ya siku nane ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman
Kinana, katika mkoa wa Lindi.
“Chama chetu
kiko imara na kinafuata kanuni na taratibu zake za kuwawajibisha wale
wanaokosea ndani ya chama, skendo zote za rushwa mnazoziskia huko
tunashughulika nazo, hata hili sakata linaloendelea huko bungeni la
Escrow, msimamo wa chama ni kuwawaliohusika waondoke waache chama kikiwa
salama,” alisema Nape.
Alisema chama hicho kinafuata maadili kanuni na miiko ya uongozi iliyopo kwenye katiba hivyo hakiwezi kulea uovu.
Nape
alitolea mfano wa utendaji kazi ndani ya chama hicho katika sakata la
Richmond, ambalo lilisababisha aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa na
mawaziri wengine wawili kujiuzulu.
Habari : Muhibu Said, Dodoma; Thobias Mwanakatwe, Dar
na Mary Godfrey, Lindi.
CHANZO: NIPASHE
Post a Comment