0
 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Seleman Jafo akifunga kikao kazi kilichohusisha Wakuu wa Mikoa,Makatibu Tawala wa mikoa na Wakurugenzi wa Idara Tamisemi leo mjini Dodoma.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Selemani Jafo amesema kuwa jumla ya viwanda 1,285 kati ya 2,600 vimejengwa katika mikoa mbalimbali ikiwa ni miezi mitatu tangu atoe agizo la ujenzi wa viwanda 100 kwa kila mkoa.

Akizungumza katika kikao kazi cha kupitia bajeti ya TAMISEMI na Mikoa, kilichofanyika leo mjini Dodoma Jafo amesema viwanda hivyo vilivyojengwa ni sawa na asilimia 49.4 na kutoa ajira.

Amesema agizo hilo bado linaendelea kutekelezwa ambapo hadi kufikia Desemba 31, mwaka huu kila mkoa unatakiwa kuwa na viwanda 100 ambavyo ni sawa na viwanda 2600.

Amebainisha kuwa kupitia wakuu wa mikoa ajenda ya Rais John Magufuli ya Viwanda inatekelezwa na kuwataka waendelee kuitekeleza.

Kwa mujibu wa Waziri Jafo, viwanda vidogo vinavyojengwa  ni vile vinavyoanzia sh.milioni 2.5 hadi sh.milioni 10.

Akizungumzia kuhusu maandalizi ya bajeti kwa mwaka huu Waziri Jafo amewataka Makatibu Tawala wa Mikoa kuhakikisha kuwa wanawapitisha vizuri Wakuu wa Mikoa ili waelewe bajeti za mikoa yao na wahakikishe kuwa randama zinakaa vizuri.

Amesema katika bajeti ya mwaka 2017/18 Ofisi ya Rais TAMISEMI pamoja na Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa walitengewa asilimia 20 ya bajeti yote sawa na Trilioni 6.8.

Naye, Kaimu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI Dk. Zainabu Chaula amewataka Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala wa Mikoa kuwa kitu kimoja katika utekelezaji wa shughuli za Serikali ili kuleta ufanisi unaotarajiwa.

Amesema ni vyema viongozi hao hasa Ofisi za Sekretarieti za mikoa kuhakikisha kuwa wanawapa taarifa sahihi Wakuu wa Mikoa ili kurahisisha utendaji wa kazi za serikali.

Awali kabla ya Jafo, Wakuu wa mikoa walitoa taarifa zao za ujenzi wa viwanda hivyo kufuatia agizo alilolitoa ambapo Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Paul Makonda alisema katika mkoa wake tangu kutolewa kwa agizo hilo viwanda 88 vimejengwa.

Hata hivyo amesema kumekuwepo na changamoto ya umeme na maji na kuiomba serikali kuliangalia suala hilo ili kuendelea kuvutia wawekezaji zaidi.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo amesema katika mkoa huo wamejenga viwanda 22 ambavyo ni vikubwa na vya kati na vingine vipo katika hatua mbalimbali za ujenzi.

“Changamoto iliyopo ni nishati ya umeme na kwa mkoa wetu tunahitaji tuwe na Megawati 800,”amesema Mkuu huyo.

Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo amesema zimetengwa hekari 307,595 kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda na hadi sasa tangu kutolewa kwa agizo la Waziri Jafo vimejengwa viwanda 45 vipya ambavyo vimetoa ajira mbalimbali.

Kadhalika, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka amesema mkoa huo unaendelea kutekeleza mkakati wake wa bidhaa moja kwa wilaya moja na kwamba tangu agizo hilo viwanda mbalimbali 18 vipya vimejengwa.

Mkuu wa mkoa wa Iringa Amina Masenza amesema viwanda vipya vilivyojengwa ndani ya agizo hilo ni 124 huku Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Zainab Tellack akisema kwake amejenga viwanda 126.

Post a Comment

 
Top