0

Na. Ahmad Mmow, Lindi.
Baadhi ya wananchi na viongozi wa kijiji cha Kiwawa kilichopo katika wilaya na mkoa wa Lindi, wameshangazwa na hatua ya halmashauri ya wilaya ya Lindi ya kuchukua na kuwakabidhi wavunaji mbao 2360 walizovuna kwenye msitu wa kijiji hicho kinyume cha sheria.

Wakizungumza  kijijini hapo, wananchi na viongozi hao walisema hawaelewi ni kigezo gani vilitumiwa na halmashauri hiyo kuwapa mbao 2360 zilizokamatwa kwenye msitu wa kijiji chao na kusababisha kijiji hicho kikose ushuru. Mjumbe wa serikali ya kijiji hicho, Ahmad Koha, alisema tarehe 15 mwezi Oktoba mwaka 2015 walikamata mbao 1000 walitoa taarifa wilayani hata hivyo kwa mshangao mkubwa mbao hizo zilichukuliwa na mvunaji.

“Tuliwapigia simu akaja ofisa misitu akasema anakwenda kuchukua gari, lakini hakurudi tena. Badala yake huyo mvunaji aliyevuna kinyume cha sheria akaruhusiwa aondoke na mbao hizo,” alisema Koha.
Mwananchi Ahmad Tendele alisema mwaka jana mwezi wa kwanza tarehe 20 walikamata tena mbao 1360 kwenye msitu huo, hata hivyo halmashauri ya wilaya hiyo kupitia idara yake ya maliasili ilizuia mbao hizo zichukuliwe na yeyote hadi itakapo tambulika zilivunwa kwenye msitu wa kijiji gani Kati ya Mputwa na Kiwawa.
“Tuliambiwa zisiondoke hadi viongozi wa Mputwa na Kiwawa wakutane. Hata hivyo ofisa aliyekuja hapa hakurudi tena, mbao hizo nazo ziliondoka bila maelezo yeyote na kwamujibu wa viongozi wetu nikwamba wamekwenda wilayani mara nyingi kuuliza namna zilivyoondolewa na hatima ya ushuru wetu. Lakini mpaka sasa hakuna chochote tunachokielewa, “ alisema Tendele.
Maelezo ya Tendele yaliungwa mkono na mjumbe wa iliyokuwa kamati ya upimaji wa hewa ya ukaa, Shaibu Mkulyungu, ambae alisema wamekwenda wilayani mara nyingi kuulizia hatima ya malipo ya zao ushuru wa mbao hizo na jinsi zilivyoondolewa bila kuwashirikisha. Alidai hata hivyo hawapati ushirikiano. Alisema sababu kubwa ni migogoro ya mipaka ambayo hadi sasa haijashugulikiwa kikamilifu. Hali ambayo inatumiwa na vijiji vingine kuwaingiza wavunaji kwenye msitu wa kijiji hicho. Kwa madai kwamba vijiji vingi vinavyokizunguka kijiji hicho vimeshaharibu na kumaliza misitu yake.

Hata hivyo mwenyekiti wa kamati ya maliasili ya kijiji hicho, Said Matata alisema hata serikali ya kijiji hicho inasitahili kubeba lawama sawa na halmashauri ya wilaya. “Kamati ya maliasili inafuata miongozo yote, ila serikali ya kijiji inasitahili kubeba lawama kwa mfano kunamvunaji alikamatwa Litandantama hata hivyo mwenyekiti alisema aachwe pamoja na vifaa vyake,” alisema Matata.

Mwanahawa Tawile ambae pia ni mjumbe wa serikali ya kijiji alisema halmashauri ya wilaya hiyo hainabudi iwaeleze sababu ya kuwaruhusu wavunaji waliovuna kinyume cha sheria waondoe mbao hizo bila kuwashirikisha, huku ikijua wenye haki na mbao hizo ni kijiji hicho. “Msitu unakwisha hakuna tunachonufaika, tunawakamata wavunaji wanatetewa nawakubwa na mbao wanapewa. Tumeanza kuvunjika moyo, huenda ndio sababu wanashindwa kushugulikia migogoro ya mipaka sababu wananufaika nayo,” alisema Mwanahawa.

Mwenyekiti wa serikali ya kijiji hicho, Issa Mtambile, licha kukanusha kuwa serikali ya kijiji hicho haihusiki na upotevu wa mbao hizo wala yeye kuamrisha mvunaji aliyekamatwa aachwe na vifaa vyake. Alisema serikali ya kijiji haikushirikishwa kuziondoa mbao hizo 2360 bali wavunaji walikuwa wanasema walikuwa wanaruhusiwa na halmashauri. Hata hivyo wanapouliza hawapati ushirikiano na hawajui hatima ya mgogoro ushuru wa mbao hizo ambazo alidai kuwa anauhakika zilivunwa kwenye msitu wa kijiji hicho.

Akijibu malalamiko hayo kwaniaba ya mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, kaimu mkuu wa idara ya maliasili, Patrick Senga alisema halmashauri imekuwa ikishugulikia migogoro ya mipaka. Ikiwamo mipaka ya Kiwawa na vijiji vilivyokizunguka. Hata hivyo tatizo kubwa ni vijiji hivyo kutoheshimu mipaka iliyopo kisheria.

Akibainisha kuwa tamaa ya maliasili ndio inayosababisha hali hiyo. Matokeo yake migogogoro imekuwa ikijirudia mara kwa mara. Kuhusu mbao zinazodaiwa kukamatwa na kuchukuliwa bila idhini ya kijiji, Senga alisema mbao hizo zilivunwa katika kijiji cha Namkongo.

“Eneo lililovunwa mbao hizo halipo Kiwawa wala Mputwa bali Namkongo, zilivunwa kwa kufuata sheria, taratibu na kanuni. Zililipiwa ushuru husika katika kijiji husika, “ alisema Senga.
Alikiri kuwa migogoro ya mipaka inaathiri mapato ya vijiji na halmashauri hiyo. Huku akibainisha kuwa baadhi ya wafanyabishara wanaitumia kuvamia na kuvuna mazao ya misitu kinyume cha sheria. Hivyo halmashauri imejipanga kuendelea kupima mipaka kwa kushirikiana na wakala wa misitu.

Post a Comment

 
Top