0

Kati ya jambo mojawapo linaloonekana ni kikwazo kikubwa hadi sasa kwa watu wengi, hasa kwa wale wanaohitaji kuingia katika biashara na kujiajiri binafsi ni juu ya namna ya kupata mtaji wa biashara.
Mtaji wa kuanzia kufanya biashara ndio umekuwa chanzo cha vijana wengi hivi leo kutoa sababu ya wao kushindwa kuingia katika biashara na kujiajiri binafsi; hasa ukizingatia hali ya sasa ya ukosefu wa ajira iliyokithiri hapa nchini.
Ukosefu wa ajira pamoja na ukosefu wa mitaji ya kuanzia kufanya biashara, umesababisha vijana wengi wanaomaliza vyuoni na wale wanaotaka kujiajiri binafsi kutumia kelele zao nyingi kulalamikia serikali na taasisi nyinginezo nchini juu ya umaskini na ongezeko la kushuka kwa kiwango cha uzalishaji.
Nami kupitia makala hii fupi ninayokuandikia leo kupitia katika mtandao huu wa Ishi Ndoto Yako; ninapenda kukupa habari njema kwako wewe kijana na mtu yoyote ambaye leo hii umeshindwa kujiajiri binafsi baada ya kumaliza masomo yako na hatimaye kubaki ukiilalamikia serikali juu ya hatma yako.
Hakuna serikali yoyote duniani inayoweza kutoa msaada wa kila kitu kwa watu wake wote ambao ni wahitaji. Ukizingatia kwamba kila panapokucha kuna ongezeko kubwa la watu hasa vijana wanaohitimu kila mwaka elimu yao ya masomo ya juu. Huku bado hakuna mahali pa kuwapeleka na kuwapa ajira.
Hivyo kwa kuliona jambo hili nimependa kukupa mwaga na habari njema ya namna ya kupata mtaji wa kuanzia biashara unayohitaji kuifanya kwa muda mrefu; uwe chuoni au nyumbani ni vyema ufahamu inakupasa utambue jambo hili ninalokwenda kukuambia sasa.
Kama wewe ni kijana au mtu unayehitaji kuanzisha biashara yako binafsi na unahitaji mtaji kwa muda mrefu; nataka utambue kwamba mtaji wa kuanzisha biashara yako unayohitaji kuanzisha haupo serikalini wala kwenye taasisi nyingine zozote zile. Bali upo kwako binafsi.
Nataka uelewe nilichosema hapo juu nikirudia tena ya kwamba; mtaji wa kuanzia biashara yako uliyo na maono na malengo nayo kwa muda mrefu tangu ukiwa chuoni hadi sasa bado ukiwa mtaani nk. upo kwako binafsi, haupo serikalini.
Usisubiri serikali ndio ikupe mtaji wa kuanzia biashara; wala usisubiri taasisi binafsi na mabenki kukukopa fedha kwa ajili ya kuanzia biashara unayoitaka. Bali badilika kwa kufahamu kuwa mtaji ni wewe binafsi na kile ulichonacho wewe binafsi.
Kwa nini nasema mtaji ni wewe binafsi? Ni kivipi wewe unaweza kuwa mtaji wa biashara unayohitaji kufanya?
Nataka utambue kuwa wewe ni mtaji wa kwanza kwa sababu kuu kubwa ambayo nimeithibitisha kwa muda mrefu na nina uhakika nayo; na hii si sababu nyingine bali ni akili, nguvu, kipaji, uwezo na ubunifu wako ulionao ndio mtaji wa kwanza wa dhidi ya kile unachotaka kukifanya.
Mambo hayo yote manne ndio mtaji wako tosha wa kwanza unaoweza kuutumia kuboresha na kuinua maisha yako; na kujua ni namna gani ya kufanya ili uweze kuwa miongoni mwa watu matajiri duniani sawa na wengine waliofanikiwa.
Jambo moja muhimu unalopaswa kufahamu ni kujua ni namna gani ya kutumia akili na maarifa yako yote, nguvu zako, kugundua na kukitumia kipaji ulichonacho, na kubuni njia na wazo bora la kukupeleka katika kilele cha mafanikio yako.
Kwa msaada wa kukujenga katika jambo hilo ninakutaka uambatanishe mambo hayo na ngunzo tatu muhimu za kukuwezesha kutimiza maono yako ambazo ni imani, uhusiaano mzuri na wengine pamoja na kutokukata tamaa juu ya kufikia maono na malengo mazuri uliyonayo.
Hadi kufikia hapo nikutakie mwanzo mzuri wa kuanza kufikiri upya juu ya maono yako uliyoyaacha kwa kuisubiri serikali na taasisi binafsi zikusaidie kuyatimiza. Usiogope! songa mbele.

Post a Comment

 
Top