Na Julias Mtatiro
Hivi
karibuni nimesaidiana kimawazo na Watanzania wenzangu katika kufanya
uchambuzi wa watu wanaotajwa au waliojitangaza kuwa watawania uteule wa
urais kupitia CCM na nalishukuru gazeti hili kwa kukubali kuchapisha
maoni yangu.
Haikuwa kazi
nyepesi na namshukuru kila mmoja aliyetoa mchango wake wa mawazo na
aliyefuatilia nilichoandika, lakini nawaomba radhi wale wote ambao
hawakupenda nilivyoandika na hasa walioumizwa lakini mrejesho mkubwa
niliopokea kutoka kwa jamii ni kuendelea kuifanya kazi hii kwa sababu
ina tija kwa Taifa.
Kabla
sijafunga ukurasa wa CCM na kuhamia kwa vyama vya upinzani niliona
nimalizie na kidokezo cha mwisho cha uchambuzi mfupi wa fikra zangu juu
ya nani anaweza kupitishwa na CCM kuwa mgombea na huenda Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, ikiwa chama hicho kitashinda uchaguzi wa mwaka
huu.
Kwa kifupi
nitajadili nanyi sifa kumi za mtu huyo kutokana na dalili na mwelekeo wa
CCM, hali inayokabiliwa nayo hivi sasa na mpasuko unaoinyemelea.
1. Anayeelewana na kukubalika kwa Rais anayemaliza muda wake
Watu wengi
niliozungumza nao wanaidharau sifa hii. Lakini bado naona kuwa CCM
itaitumia kumpata mgombea. Watu wengi walijaribu kuniambia kuwa hata
mwaka 1995, Benjamin Mkapa hakuwa chaguo la Ali Hassan Mwinyi na kwamba
hata mwaka 2005, Jakaya Kikwete hakuwa chaguo la Mkapa na kwamba mwaka
2010 pia Kikwete hatapata chaguo lake.
Lakini
nasisitiza kuwa nyakati zinabadilika sana na huenda CCM ikapitisha
mgombea ambaye anaweza kuwa chaguo la Kikwete kwani Rais huyo anaifahamu
CCM vizuri na amefanya mambo mengi katika siasa za chama hicho.
Hatari ya sifa hii
Chama
kinapopitisha mgombea kwa sababu tu anafahamiana na kukubalika na
kiongozi anayemaliza muda wake, huwa kuna hatari ya mpasuko mkubwa ikiwa
wagombea wengine hawataridhishwa na upendeleo aliopewa mwenzao na hivyo
wanaweza kufanya uamuzi wa kuondoka katika chama hicho.
2. Mchapakazi na mwadilifu lakini atakayekubali kusikiliza mahitaji na matakwa ya CCM
CCM
inahitaji mgombea mchapakazi na mwadilifu ili kuziba baadhi ya mashimo
yaliyoachwa na Serikali inayoondoka kwa haraka na lengo la kufanya hivi
ni kuhakikisha kuwa wananchi wanaendelea kukiamini na labda kukiunga
mkono. Lakini CCM ya sasa bado inahitaji sana msaada wa Dola ili
iendelee kuwa madarakani. Kuna wakati Rais Kikwete mwenyewe aliwahi
kuwatamkia wana CCM kuwa wanafanya kazi kwa kutaka kusaidiwa na vyombo
vya dola.
Hatari za sifa hii
Hatari
iliyopo ni uendelezaji wa mambo yaleyale ambayo yamekikumba chama hicho
kwa miongo kadhaa iliyopita. CCM inahitaji mtu mwadilifu, mchapakazi na
ambaye atakataa kabisa kusikiliza matakwa ya chama chake ili ajenge
uchumi imara wa nchi, nidhamu kwa watendaji wa Serikali na kusimamia
maendeleo ya Taifa huku akiweka “Taifa Mbele na chama baadaye”. Mgombea
wa CCM ambaye atakesha akitekeleza matakwa ya CCM hatakuwa tofauti na
wenzake kadhaa waliopita.
3. Aliyekulia katika chama na anakijua vizuri
Naiona CCM
ikimpitisha mgombea ambaye anakijua vizuri chama hicho na hasa
aliyekulia ndani ya chama ikiamini kuwa atakuwa na uwezo mzuri wa
kupambana na kuzikabili changamoto za kichama na za kiserikali huku
akijua anachokifanya kwa masilahi ya chama na serikali.
Hatari ya sifa hii
Katika dunia
ya leo ambayo vyama vinavyoendelea vinajaribu pia kutenganisha mamlaka
ya kichama na kiserikali na hata kuwa na watu tofauti katika uongozi wa
nchi na ule wa chama, sifa hii inajimaliza yenyewe.
Kwa sababu
watu waliokulia ndani ya chama hicho ndiyo wamekuwa wakijenga makundi
makubwa, kujuana, kupendeleana na kufumbiana macho, ukiniuliza nitasema
CCM ya sasa inahitaji mtu “atakayekuwa anamuua nyani kwa kumfumbia
macho”.
Yaani CCM
inahitaji mtu asiyekulia ndani ya chama hicho na asiyejua ‘uhafidhina’,
‘uswahili’ wa wanaojiita “wenye chama”. Kwa lugha ya mtaani, chama hicho
kinahitaji ‘mgombea kauzu’ na anayeweza kusimamia mambo ya nchi kwa
matakwa ya raia bila kuyumbishwa na matakwa ya chama hicho, kama hayana
tija. Mtu wa namna hii hawezi kuwa aliyekulia ndani ya CCM.
4. Mzoefu wa kufanya kazi nchini
Naiona sifa
hii kama muhimu kwa CCM na isiyo na hatari kubwa. Kwamba inaweza kumteua
mgombea mwenye uzoefu mkubwa katika kufanya kazi serikalini lakini awe
anakijua chama hicho vizuri. Mtu wa namna hii anaweza kuwa na tija kwa
chama hicho hasa ikiwa rekodi zake za utumishi ni nzuri na zenye tija.
5. Asiye na makundi na anayejua mahitaji ya makundi yanayosigana
Natambua
kuwa tunakubaliana CCM iko kwenye mpasuko unaotokana na makundi na chama
hicho hakina namna ya kufanya zaidi ya kuteua mgombea asiye na makundi
na ambaye atakubaliwa na makundi mengine lakini ambaye ikiwa
atachaguliwa, ataweza kuyalea makundi hayo kwa sababu anajua mahitaji
yao na labda ataweza kutoa mahitaji ya makundi hayo ili kuyafanya
yatulie na kutoisumbua Serikali na chama hicho.
Katika dhana hii ndipo wale wagombea ‘neutral’ huingia na kupata fursa ya kutuliza hali ya mambo.
Hatari ya sifa hii
Mgombea
atakayeteuliwa kwa dhana ya kuwa ‘neutral’ anaweza kuwa hasimu mkubwa wa
moja ya makundi yanayosigana na mapambano ya kutomuunga mkono
yakaendelea. Au, mtu huyo atakayeteuliwa anaweza kuwa dhaifu kimtandao
na kiuwezo kuliko yalivyo makundi yanayopambana. Kitakachojitokeza ni
mpasuko mkubwa zaidi kuliko ambao ulikuwa unatatuliwa na huu wa pili
unaweza kabisa kukosa mtu wa kuutatua. Kwa mtazamo wangu CCM, ilihitaji
mgombea ambaye akiingia atasambaratisha makundi yote na labda kukiacha
chama hicho ‘kipumue’.
6. Anayeweza kukemea rushwa huku akiilinda CCM
Naweza
kuthubutu kusema kuwa tangu alipoondoka Mwalimu Nyerere, CCM haijawahi
kupata mgombea na hata kiongozi wa nchi aliyeonyesha nia ya dhati, moyo,
malengo, kiu na uwazi katika mapambano dhidi ya rushwa. Moja ya mambo
ambayo yanakiweka chama hicho kwenye hali mbaya kisiasa mwaka huu ni
tuhuma kubwa za rushwa na ufisadi.
Hakika hapa
ndipo CCM ilipo na mtihani mgumu zaidi, kwamba inaipasa kuteua mgombea
msafi sana na asiye na madoa na ambaye anaichukia rushwa kuliko kifo na
ameonyesha uwezo wa kupambana na rushwa katika rekodi zake, maneno yake
na vitendo vyake.
Hatari ya sifa hii
CCM inapaswa
kuita ‘nyeusi kama nyeusi na nyeupe vivyo hivyo’ kwenye Uchaguzi Mkuu
wa mwaka huu. Huu ni uchaguzi wa uamuzi pia na wa kuleta mapinduzi
makubwa katika nchi na ushindani mkubwa kupita wakati wowote ule. Huu si
mwaka wa kutaka mgombea mwadilifu na mpambanaji wa rushwa na wakati
huohuo kutaka akilinde chama chake. CCM inahitaji mgombea ambaye atakuwa
tayari hata kurudisha kadi ya CCM ikiwa chama chake kitaonekana
kinaendekeza mtindo wa kutaka kulindwa kwa watu wake na kwa chama katika
tuhuma kubwa za ufisadi na rushwa. Kufanya kinyume na hapo kutaendeleza
yaleyale yaliyowakatisha Watanzania tamaa kwa miongo kadhaa iliyopita
na adhabu yake kwa mwaka huu inaweza kuwa kubwa.
7. Maarufu, anayekubalika na anayeweza kuwa mshindi
CCM
itahitaji mgombea ambaye yeye mwenyewe pia ni mtaji tosha wa kupata
kura. Mwaka 2005 wakati chama hicho kilikuwa taabani kisiasa, kilikuja
kuamshwa na nguvu, umaarufu na kukubalika kwa Jakaya Kikwete,
kikajiandaa na ushindi wa kimbunga pamoja na kwamba kilisaidiwa sana na
mifumo ya dola. Mwaka huu pia nadhani CCM itahitaji mtu wa namna hiyo
‘kama yupo’ ili kukiokoa. Maana ukizunguka vijijini unaona wananchi
walivyochoka na wanavyohitaji mabadiliko.
Hatari za sifa hii
Kuteua
mgombea maarufu kuliko chama kuna faida tu wakati wa kupiga kura na
kushinda. Mara nyingi hakuna faida wakati wa kutekeleza ajenda za chama
na kuwaletea maendeleo wananchi.
Sote
tunakubaliana kuwa miaka 10 ya Kikwete imekuwa ya suluba kubwa, kwa mara
ya kwanza tumeshuhudia (hasa miaka yake mitano ya mwisho), nchi
ikishindwa kutekeleza baadhi ya bajeti za wizara kwa asilimia 50, fedha
za miradi ya maendeleo zikitolewa kwa asilimia hadi 30 au 40 huku
asilimia 70 hadi 60 zikikosekana katika miradi mingi, kuporomoka kwa
uchumi, kuporomoka kwa shilingi na mambo mengine.
Inawezekana
kuwa miaka 10 iliyopita Watanzania walichagua mtu maarufu na
anayekubalika lakini hawakuangalia ana uwezo kiasi gani kuondoa
umaskini, kuleta maendeleo, kurudisha nidhamu na uwajibikaji serikalini
na kulinda kazi za raia. Kwa hiyo, yanayotokea leo, huenda ni madhara ya
kuchagua mtu maarufu bila kuangalia umaarufu ule una tija gani kwa
maendeleo na mahitaji ya Taifa.
8. Mwenye umri wa kati, msomi, mtulivu/mpole na mwenye busara
Katika
kuweka hali ya mambo sawa, huenda CCM ikateua mgombea kwa sababu ya sifa
hizi. Mtu wa umri wa kati ili kuwavutia vijana, wanawake na wazee
(makundi yote ya kijamii) na katika chaguzi nyingine zote za nyuma CCM
ilipitisha wagombea wake wakiwa na umri wa kati (chini ya miaka 60) na
kufanikiwa.
Lakini pia,
CCM inaweza kupitisha mgombea msomi ili aendane na kasi ya utendaji ya
mabadiliko ya dunia na kuweza kuanzisha uongozi wa kisasa. Mahitaji ya
kiongozi mwenye busara yanatokana na sababu kuwa nchi hii ni kubwa
(Tanzania inalingana na nchi zote za Ulaya Magharibi, zikiwekwa pamoja).
Hii ni nchi
yenye changamoto nyingi na viashiria vya migogoro vinavyoshika kasi.
Inahitaji mtu mwenye busara za kutosha kuweza kuipeleka mbele.
Hatari ya sifa hii
Pamoja na
mahitaji ya kiongozi mtulivu na mwenye busara, kiongozi huyo anapaswa
asiwe mpole hata kidogo. Taifa letu lilipofika linahitaji rais mwenye
sifa zozote zile lakini lazima awe mkali kama pilipili pale watendaji
wanapojaribu kupindisha mambo fulani.
Asiishie tu
kuwa mkali, pia achukue hatua stahiki kila mambo yanapoborongwa. Watu
wengi ambao tunaambiwa wana busara kila nikiwaangalia nawaona kama
wapole. Inawezekana kabisa kuwa Watanzania wengi wanaona kama busara na
upole ni vitu vinavyokwenda pamoja.
Watu wapole
wana matatizo makubwa katika usimamizi na kwa hakika binadamu anapaswa
awe mpole katika mazingira yanayohitaji upole lakini awe mkali katika
mazingira yanayohitaji ukali wa kiwango hichohicho.
9. Anayeweza kuupigania Muungano wa Serikali mbili kwa dhati
Sifa hii
nayo isidharauliwe. Kwamba CCM itaitegemea katika kumpata mgombea urais
wake. Tukumbuke kuwa CCM haiwakubali na kuwaamini viongozi wanaotaka
Muungano nje ya mfumo wa Serikali mbili. Ndiyo kusema kuwa CCM kwenye
suala la Muungano haitaki mjadala na haitaki wananchi wajiamulie
wanataka wa namna gani.
Nasisitiza
kuwa CCM inamtaka mtu ambaye anataka Muungano wa serikali mbili uendelee
na si kinyume na hapo. Hii ni sera ya CCM na inaamini kuwa lazima
iendelee kutekelezwa na wananchi wote tena bila kujali kuwa nchi hii
sasa ina vyama vingi.
Hatari ya Sifa hii
Kitakachojitokeza
ni kuwa, wananchi wengi wanaotaka kuwe na mjadala wa kitaifa wa muundo
wa muungano wataendelea kudhibitiwa na hata kuonekana kama maadui wa
Taifa kwa jambo la kimtizamo tu.
Kama nchi
itatumia nguvu nyingi, akili nyingi na kila rasilimali kupigania mfumo
wa serikali mbili na kusahau kuwa mahitaji makubwa ya wananchi ni
maendeleo, naona CCM itazidi kushuka thamani na kupoteza mwelekeo. Kwa
maoni yangu, CCM ingesaidiwa zaidi na mgombea ambaye atakuja na mtazamo
huru juu ya muungano, hasa yule ambaye atakuwa tayari kuanzisha mjadala
wa kitaifa ili wananchi waamue wanataka muungano wa namna gani.
Lakini pia,
kuwaacha wagombea ambao wana sifa kubwa kuongoza nchi eti kwa sababu tu
hawaamini sana katika serikali mbili itakuwa ni makosa makubwa. Sababu
hii inaweza kukifanya chama hicho kichague mgombea mbovu kwa sababu
atalinda serikali mbili.
10. Mwenye uzoefu na masuala ya kimataifa
Kwamba kwa
namna dunia ilivyokumbwa na migawanyiko, mitanzuko na hata mabadiliko
makubwa ya kidiplomasia, huenda CCM ikahitaji mtu mwenye uzoefu mkubwa
wa masuala ya kimataifa kwa ngazi na kiwango ambacho chama hicho kitaona
inafaa. Lengo litakuwa ni kuhakikisha kuwa nchi yetu inaendelea kufanya
vizuri, kuheshimika na kuungwa mkono na jumuiya ya kimataifa.
Hatari ya sifa hii
Watu wengi
waliobobea katika masuala ya kimataifa na kidiplomasia huamini katika
dhana ya kushughulika kimataifa, kusafiri sana, kusaka misaada na
marafiki kimataifa n.k. Ndiyo maana serikali inayomaliza muda wake
imetumia muda mkubwa kufanya masuala ya kimataifa lakini hadi naindikapo
hali ya nchi kimaendelea, kiuchumi na kijamii ndiyo kwanza inazidi kuwa
mbaya.
Nadhani
Taifa la Tanzania ya sasa linahitaji mtu mweledi wa kiwango cha kutosha
kuweza kuongoza nchi na ambaye atakuwa na uwezo mkubwa zaidi katika
kutengeneza fursa pana za kiuchumi ndani ya nchi, ambaye ataweza
kuhamasisha wafanyabiashara wa ndani ya nchi wawekeze katika viwanda
vidogovidgo na Serikali iwasaidie kusimamia sehemu ya mitaji ya viwanda
vikubwa. Taifa linahitaji mtu ambaye atatumia muda wake mwingi akiwa
mikoani na ofisini akisimamia utekelezaji wa maendeleo ya nchi yeye
mwenyewe kuliko kusafiri kila uchwao kwenda nje ya nchi.
Kwa mtizamo
wangu, kubobea katika masuala ya kimataifa huku ukikosa weledi muhimu wa
namna ya kupandisha uchumi wa Taifa na wananchi ukiwa hapahapa ndani –
hakuna tija yoyote katika Taifa maskini kama Tanzania.
Hitimisho:
Huu ni mwaka
wa kusuka au kunyoa kwa CCM, chama hicho kikongwe huenda kinakabiliwa
na changamoto kubwa kuliko wakati wowote ule kihistoria. Nguvu ya vyama
vya upinzani imekuwa kubwa na haina mfano. Makosa ya CCM katika uteuzi
wake ni jambo muhimu kwa vyama vya upinzani na ni suala la kujutia kwa
CCM.
Sifa za
mgombea wa CCM zina maana kubwa kama karata ya kutafuta ushindi wa chama
hicho, na naamini kuwa kwa mwaka huu, kama CCM itaondoka madarakani,
basi sababu mojawapo inaweza kuwa aina ya mgombea iliyempitisha.
Hata hivyo,
nawatakia wana CCM na Watanzania wote tafakuri nzito juu ya mteule wake
ambaye lazima tuseme ukweli kuwa, ikiwa atashinda uchaguzi, ndiye
atakuwa Rais wetu wa awamu ya tano.
CREDIT: MWANANCHI
Post a Comment