0
                              
Dar es Salaam. Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imezitaka kampuni za simu nchini kufuata sheria wanapotaka kufanya mabadiliko ya tozo za huduma zao ili kutoleta mshtuko kwa wateja.
Kauli hiyo imetolewa ikiwa ni siku chache tangu kampuni za Vodacom, Airtel na Tigo kupandisha bei za vifurushi vya muda wa maongezi vinavyojumuisha pia ujumbe mfupi na intaneti.
Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Profesa John Nkoma alisema hayo jana kupitia matangazo yaliyochapishwa katika vyombo vya habari.
Alisema kampuni za simu zinapaswa kutuma mapendekezo ya mabadiliko ya bei katika  mamlaka hiyo kabla ya kutekeleza bei mpya inayoendana na gharama zao za uendeshaji.
“Kampuni hizo zinapaswa kutoa machaguo kwa kila kifurushi wanachotoa ili mteja awe na uhuru na kulipia akitakacho,” alisema na kuongeza. “Wapo wanaotaka kuongea tu. Wengine wanataka kutuma ujumbe. Na baadhi wanataka intaneti. Kwa kiwango fulani cha fedha kuwepo na machaguo hayo yote ili kila mmoja alipie kinachomfaa.
Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mbarawa alisema Serikali inasubiri mapendekezo ya TCRA kabla ya kufanya uamuzi kuhusu sakata hilo.
“Wao ndiyo wenye mamlaka ya kutoa muongozo na baada ya kufanya hivyo hutoa ushauri kwetu. Kuanzia Septemba bei itashuka kwa kuwa ushindani utaongezeka baada ya kampuni ya Viatel kuanza kutoa huduma. Kwa sasa wanajenga miundombinu...watasambaza intaneti ya 3G mpaka vijijini,” alisema.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom, Rene Meza alikaririwa akisema kuwa ongezeko hilo limesababishwa na ongezeko la kodi, hivyo walichukua hatua hiyo ili kuepuka hasara.

Post a Comment

 
Top