Dar es Salaam. Mfumuko wa bei kwa mwezi januari umeshuka
hadi kufikia asilimia 4.0 kutoka asilimia 4.8 ya Desemba mwaka jana
kutokana na kupungua kwa bei za bidhaa mbalimbali ikielezwa kwamba
kupungua huko kulikuwa hakujatokea kwa miaka miwili iliyopita.
Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Takwimu za Jamii,
Ephraim Kwesigabo alieleza kuwa kushuka huko kumetokana na kupungua kwa
kasi ya upandaji bei ya bidhaa na huduma ikilinganishwa na ilivyokuwa
Desemba .
Amesema mfumuko wa bei za vyakula na vinywaji umepungua hadi asilimia 4.9 kutoka asilimia 5.7 ya mwezi Desemba.
Ametaja baadhi ya vyakula vilivyochangia kushusha
mfumuko huo kuwa ni mahindi yaliyoshuka kwa asilimia mahindi 13.3, unga
wa mahindi (6.2), samaki (2), ndizi za kupika (11.3), mihogo (12.0)
Kwa mujibu wa Kwezigabo bidhaa zisizo za chakula
nazo zilipungua. Mafuta ya taa yalishuka kwa asilimia 8.4, dizeli
(10.2), petroli (6.8) na gesi ya kupikia ilishuka kwa asilimia 2.9.
Takwimu hizo mpya zinaonyesha kuwa fahirisi za bei zimeongezeka kutoka
146.0 Januari 2014 , hadi kufikia 152.43 Januari mwaka huu.
“Bidhaa zisizo za vyakula kama vile mavazi ya
wanawake,mkaa na kodi nazo zimechangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa
fahirisi katika mwezi huu”amesema Kwezigabo
Amefafanua kuwa mfumuko wa bei unaopimwa kwa
kipimo cha mwezi hadi mwezi umeongezeka kwa asilimia 2.0 ikilinganishwa
na ongezeko la 0.2 Desemba mwaka jana.
Post a Comment